Saratani ya Ovari inavogharimu waliochelewa kuzaa, wanene kuondolewa kizazi

      Comments Off on

Saratani ya Ovari inavogharimu waliochelewa kuzaa, wanene kuondolewa kizazi

Ni saratani nadra kutokea duniani, mwanamke mwenye saratani hii {ovarian cancer} mara nyingi huchelewa kugundulika mapema na hata wale wachache wanaogundulika hukutwa ugonjwa umefikia kiwango cha juu, ngumu kutibika.
Hali hiyo husababisha wengi wao kuishia kung’olewa kabisa mji wa mimba {uterus}kwani saratani hiyo hukutwa imesambaa na kuathiri kwa kiwango kikubwa.
Wanawake ambao hawajazaa kabisa au wale waliochelewa mno kuzaa juu ya umri wa miaka 35 wanatajwa kwamba ndilo kundi lililopo kwenye hatari na uwezekano mkubwa wa kupata saratani hii.


MATUKIO NA MAISHA BLOG imefanya mahojiano haya maalum na madaktari bingwa wa magonjwa ya saratani katika Taasisi ya Saratani Ocean Road, wanafafanua kwa undani kuhusu saratani hii…
Kulingana na takwimu za Taasisi ya Saratani Ocean Road kumekuwa na ongezeko kidogo la wanawake wanaopokewa wakikabiliwa na saratani ya ovari, rekodi inaonesha katika mwaka 2006 kulikuwa na wanawake 21 kwa mwaka waliokuwa wanatibiwa kufikia mwaka 2014 idadi iliongezeka hadi wanawake 49.
Idadi hiyo ni sawa pungufu ya asilimia moja ya wagonjwa wote ambao walionwa kwenye taasisi hiyo katika kipindi hicho cha miaka minane mfululizo na kwamba idadi inaonesha kila mwaka ni takribani wagonjwa wapya wa saratani hiyo ni wanawake 40 hadi 50 wanaofika kupatiwa matibabu ndani ya taasisi hiyo.
“Pamoja na kwamba ni saratani nadra lakini ni ngumu kutibika, mtu anapogundulika kuwa nayo,” anasisitiza Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Saratani wa ORCI, Emmanuel Lugina.
Dk. Lugina anasema tathmini ya Ocean Road inaonesha wanawake wanaofika kupatiwa matibabu wengi ni watu wazima wenye umri kuanzia miaka 50 na kuendelea.
“Inaweza kurithiwa {yaani} ikiwa mama yako aliwahi kuugua upo kwenye hatari ya kupata, wenye unene kupita kiasi wapo hatarini kupata saratani hii, wengine ni wasomi, ambao wamechukua muda mrefu kwenye masomo hawajazaa au wamezaa mtoto mmoja.
“Kadri unavyoongeza idadi ya watoto inakuwa kinga dhidi ya saratani ya mayai, lakini hatuwezi kumpangia, kuna masuala ya uchumi na mwenuyewe alivyopangilia, ila tafiti zinaonesha ukiwa na watoto wengi hatari ya kupata saratani hii inakuwa inapungua,” anabainisha.

Anasema asilimia kubwa ya wagonjwa wanaowatibu ni wanene, unene uliochangiwa na sababu mbalimbali kutokea, ikiwamo ulaji usiofaa, wanakula vyakula vyenye mafuta mengi ambavyo si mlo kamili na hawajishughulishi kwa mazoezi.
“… Mwisho wa siku wanakuwa na uzito mkubwa, mafuta yanaongezeka mengi chini ya ngozi, haya mafuta yana uwezo wa kubadilisha zile homoni {eostrejeni na …. na kuathiri yale mayai,” anasema.
Dk. Lugina anafafanua kwamba usipofanya mazoezi, ukala vyakula vya mafuta, unakuwa mnene na hivyo kuongeza mafuta chini ya ngozi.
“… na mwili una namna ya kugeuza yale mafuta yakawa homoni za kike na baadae yana uwezo wa kuathiri zile ovari, unene uliozidi ni nchanzo kikubwa si tu cha saratani bali magonjwa mengine sugu.
“Unachangia saratani nyingi pia kama ya utumbo mpana, tezidume, matiti kwa wanaume ni kutokana pia na unene,” anasisitiza Bingwa huyo.


MFUMO WA OVARI
Ovari ni miongoni mwa jozi muhimu za viungo ndani ya mwili wa mwanamke kukamilisha mfumo wake wa uzazi, kimaumbile huwa zipo mbili, moja upande wa kulia na nyingine kushoto mwa mfuko wa uzazi {uterus}.
Kutoka kwenye mfumo wa uzazi hadi kwenye ovary kuna mirija ya falopio ambayo hii ndiyo kiunganishi kikuu, ovari zenyewe huwa katika ‘kaviti’ ya pelviksi na hujishikiza kwenye ligamenti mbili.
Ligamenti hizi ni tishu za kuunganisha zenye nyuzi na uwezo wa kupinda ambazo hushikilia viungo mbalimbali vilivyopo ndani ya mwili kadhalika kuunganisha mfupa mmoja na mwiline kwenye jointi.
Kibaiolojia zina kazi mbalimbali kuu ikiwa kutengeneza mayai ya kike ya uzazi, kuzalisha homoni mbalimbali za kike ikiwamo estrogeni ambayo ina kazi muhimu ya kukuza na kukomaa kwa viungo vya uzazi, kurekebisha na kuwezesha mzunguko sahihi wa hedhi, kuwezesha tabia za kike mfano kuota maziwa na kutanuka nyonga nakadhalika.
Aidha ina kazi ya kumpa mwanamke hisia za tendo la kujamiiana, huku homoni nyingine ya ‘projesteroni’ nayo ikizalishwa humo kwa ajili ya kufanya kazi ya kuandaa mfuko wa uzazi kumtunza mtoto akiwa tumboni mwa mama na hata kuzuia mimba isiharibike baada ya kuundwa.
Zipo pia homoni nyinginezo ambazo huzalishwa katika vifuko vya ovari ikiwamo ile ya relaxin ambayo hufanya kazi ya kuongeza ulaini wa mifupa na misuli ya nyonga wakati wa ujauzito ili kusaidia mtoto atoke kirahisi wakati wa kujifungua.
Mkurugenzi wa Huduma za Kinga ya Saratani Ocean Road, Dk. Crispin Kahesa anafafanua kwamba saratani hiyo inakadiriwa kuchukua asilimia 1.7 ya saratani zote duniani kulingana na Shirika la Afya Duniani (WHO).
Anasema ni ngumu kugundua saratani ya ovari katika hatua za awali kwani huwa haioneshi dalili za wazi ambazo muhusika anaweza kuhisi kuna tatizo linalomkabili.
“Walio wengi wanafika ikiwa imesambaa kwenye tumbo la uzazi, tumbo kubwa na sehemu ya mfuko wa uzazi,” anabainisha.


MABADILIKO YANAVYOANZA
Kahesa ambaye pia ni Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Saratani anasema yapo mabadiliko kadhaa ambayo muhusika huyapata na wengi huwa hawayatilii shaka kwamba huenda kuna kitu ambacho hakipo sawa mwilini mwao.
“Kubwa ni kubadilisha mfumo wa chakula, kwa njia ya kwenda haja, labda ulizoea asubuhi unapata {‘choo’}, unakuta inabadilika.
“Anaona tumbo limejaa, wengine anakuwa anacheua, inaambatana na maumivu ya tumbo, kupoteza hamu ya kula, kwa muonekano tumbo lake huwa kubwa.
“Hasa kutokana na maji yanakuwa yapo eneo la tumbo, anajisikia mwili kuishiwa nguvu na kupoteza uzito kwa sababu hamu ya kula inakuwa imeisha”.
“Dalili nyingine huwa zinatokana na kiwango ambacho ugonjwa umefikia, kama ni hatua za juu sana ugonjwa unaleta madhara kwenye ini kwa hiyo atakuwa na dalili zinazonesha ini au figo limefeli,” anasema.


USHAURI
Dk. Kahesa anasema jambo jingine la muhimu wanaloshauri kuzingatiwa ni kina mama kupata mimba katika umri ambao usizidi miaka 35 ili kuweza kuepuka saratani hii .
“Walio wengi mimba hatarishi ni zile zinaanzia miaka 35 na kuendelea, kama ilivyo mimba hatarishi kwenye umri mdogo, ni zile chini ya miaka 25,
“Tunaamini ukamilifu wa mama ni miaka 25, hatari inaonekana kadri umri unavyoenda, mimba ya kwanza {35}huu ni umri mwafaka,” anashauri.
Kuhusu matibabu, Dk. Kahesa anasema huhusisha pande mbili ikiwamo upasuaji wa kuondoa uvimbe ulipo au tiba ya dawa za kemia.
“Wengi wapo hatua za juu hupatiwa tiba mchanganyiko au mojawapo kati ya hizo. Tiba nyingine zinahusiana na kuondoa kizazi.
“… atakuwa na maumivu atahitaji dawa za kumsaidia kupunguza maumivu, atahitaji dawa za kumsaidia kumpa hamu ya chakula, atakuwa amedhoofu atahitaji tiba lishe,” anabainisha Dk. Kahesa.