Maadhimisho ya siku ya saratani duniani

      Comments Off on

Maadhimisho ya siku ya saratani duniani

Katika kuadhimisha Siku ya Saratani Duniani, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeendelea kuhimiza jamii kuchukua hatua madhubuti za kujikinga dhidi ya saratani na magonjwa mengine yasiyoambukiza.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi mtendaji wa Taasisi ya Saratani Ocean Road Dkt. Diwani msemo leo Februari 4, 2026 alipowasilisha hotuba ya waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa ambaye alitarajiwa kuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya siku ya saratani duniani katika katika viwanja vya Taasisi ya Saratani Ocean Road.

Dkt. Msemo amesema kuwa ili kuthibiti magonjwa yasioambukiza, watanzania wanatakiwa kubadilisha mtindo wa maisha ili kuimarisha afya ikiwemo kufanya mazoezi ya mwili angalau dakika 30 mara tano kwa wiki, kupunguza matumizi ya vilevi na kuacha kabisa matumizi ya tumbaku.

Aidha, Dkt. Msemo amesema Serikali inaendelea kuhimiza wananchi kujiunga na mfumo wa bima ya afya kwa wote, ili kuwezesha uchunguzi na matibabu ya mapema kabla ugonjwa haujafikia hatua hatarishi

Ushirikiano kati ya Serikali, wataalamu wa afya, viongozi wa dini, taasisi za kijamii na vyombo vya habari umetajwa kuwa nguzo muhimu katika kufikisha elimu sahihi kwa jamii.

Maadhimisho ya Siku ya Saratani Duniani yanatumika kama wito wa pamoja kwa Watanzania wote kuendelea kushiriki kikamilifu katika mapambano dhidi ya saratani, kwa kubadili mtindo wa maisha, kuhamasishana kufanya uchunguzi wa mapema, na kuungana kwa pamoja kudhibiti saratani na magonjwa mengine yasiyoambukiza kwa mustakabali wa taifa lenye afya bora.

Waziri wa Afya Mhe Mohammed Mchengerwa mapema leo tarehe 02/02/2026 amezindua rasmi matumizi ya mashine aina ya PET CT – Scan ambapo pamoja na uzinduzi huo, ameshuhudia mgonjwa wa kwanza baada ya uzinduzi wa mashine hiyo.

      Comments Off on

Waziri wa Afya Mhe Mohammed Mchengerwa mapema leo tarehe 02/02/2026 amezindua rasmi matumizi ya mashine aina ya PET CT – Scan ambapo pamoja na uzinduzi huo, ameshuhudia mgonjwa wa kwanza baada ya uzinduzi wa mashine hiyo.

Waziri wa Afya Mhe Mohammed Mchengerwa mapema leo tarehe 02/02/2026 amezindua rasmi matumizi ya mashine aina ya PET CT – Scan ambapo pamoja na uzinduzi huo, ameshuhudia mgonjwa wa kwanza baada ya uzinduzi wa mashine hiyo.

Akizungumza katika uzinduzi huo Mhe. Mchengerwa amesisitiza kuwa anatamani kuona mashine hizi zinatunzwa na kuenziwa kwani ndio nembo pekee za maendeleo kwenye sekta ya Afya.

Mhe. Mchengerwa amesema kuwa uwepo wa mashine hii ya PET CT – Scan nchini kwetu utaokoa pesa nyingi sana kwani safari za kwenda India kufuata mashine hii, zilikuwa zikiwagharimu watanzania kiasi cha shilingi milioni 6 mpaka milioni 8, lakini kwa hapa ORCI itakuhitaji kuwa na shilingi milioni moja na laki mbili tu ili kuweza kupata huduma hii kwa haraka huku ikitolewa kwa kiwango cha kimataifa sawasawa na nchi zilizoendelea.

Aidha amewataka watumishi wa ORCI na watanzania kwa ujumla kuendelea kuiamini serikali yao na wakiwa kama wasomi waishike nchi yao kuendeleza uzalendo ili serikali iweze kutulia na kufanya mambo makubwa zaidi ya hayo.

Katika hatua nyingine Mhe. Mchengerwa amempongeza mkurugenzi mtendaji wa Taasisi ya Saratani Ocean Road kwa kasi kubwa ya maendeleo anayoifaya na kuongeza kuwa ORCI ndio Taasisi ya kwanza kwa Taasisi zote za kiafya nchini, kutekeleza maagizo yote aliyoyatoa kwa Asilimia Mia moja.

Nae Mkurugenzi mtendaji wa Taasisi ya Saratani Ocean Road Dkt. Diwani Msemo, amemshukuru Mhe. Mchengerwa kwa kutambua juhudi kubwa ambazo Taasisi hiyo inazifanya katika kuboresha huduma za Afya nchini hususan kwa wagonjwa wa Saratani nchini huku akiahidi kufanya mambo makubwa zaidi ili kuleta mabadiliko ambayo hayakuwahi kutokea nchini Tanzania kwenye sekta ya Afya.

Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa azindua rasmi Bodi ya wadhamini ya Taasisi ya saratani ocean road

      Comments Off on

Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa azindua rasmi Bodi ya wadhamini ya Taasisi ya saratani ocean road

Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa leo amezindua rasmi Bodi ya wadhamini ya Taasisi ya saratani ocean road, katika hafla fupi iliyofanyika katika ukumbi wa Mwalimu Nyerere uliopo katika Taasisi hiyo.

Akizungumza na wajumbe wa bodi hiyo, mwenyekiti pamoja na menejiment, Mhe. Mchengerwa amewataka kudumisha mshikamano baina yao katika kutekeleza majukumu ya Bodi pamoja kupeana mawazo yatakayosaidia kusukuma mbele gurudumu la Taasisi hiyo.

Mhe.Mchengerwa ameipongeza bodi iliyomaliza muda wake pamoja na menejimenti ya Taasisi hiyo kwa kutekeleza yale yaliyoazimiwa katika Kipindi kilichopita, huku akitoa pongezi za kipekee kwa Mwenyekiti wa bodi Prof. Ephata Kaaya kwa kuteuliwa tena na Raisi kuendelea kuwa Mwenyekiti wa Bodi hiyo ya Taasisi ya saratani ocean road.

Aidha Mhe. Mchengerwa amejionea uwekezaji uliofanyika katika Taasisi hiyo zikiwemo mashine mbalimbali zilizopo za uchunguzi na matibabu ya saratani zilizosimikwa katika kipindi kilichoongozwa na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan, huku akitoa pongezi za dhati za usimamizi madhubuti unaofanywa na Mkurugenzi Mtendaji Dkt. Diwani Msemo katika kuboresha Taasisi ya saratani ocean road.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi Prof. Ephata Kaaya amemshukuru Mhe. Mchengerwa kwa kuja kuzindua Bodi hiyo huku akiahidi kutekeleza maelekezo yote yaliyotolewa na waziri pamoja na kufanya ubunifu mbalimbali katika kuboresha huduma zaidi za Taasisi ili iweze kusonga mbele kwa kasi ya serikali ya awamu ya sita.

Nae Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya saratani ocean road Dkt. Diwani Msemo amesema kuwa kutokana na uwekezaji uliofanywa na serikali katika ununuzi wa mashine nyingine za tiba mionzi itapelekea kupunguza muda wa kusubiri kwa matibabu hayo kutoka wiki ishirini mpaka wiki mbili, kwani kwa sasa mashine zitakuwa za kutosha, hivyo itaboresha utoaji wa huduma hiyo.

Rais wa umoja wa visiwa vya Comoro Bw. Azali Assoumani ametembelea kambi maalum ya madaktari bingwa iliyofika katika mji wa Anjouan na kuzungumza na madaktari

      Comments Off on

Rais wa umoja wa visiwa vya Comoro Bw. Azali Assoumani ametembelea kambi maalum ya madaktari bingwa iliyofika katika mji wa Anjouan na kuzungumza na madaktari

Mapema Leo Rais wa umoja wa visiwa vya Comoro Bw. Azali Assoumani ametembelea kambi maalum ya madaktari bingwa iliyofika katika mji wa Anjouan na kuzungumza na madaktari hao.

Akizungumza mara
baada ya kukutana na madaktari hao, Bw. Assoumani amesema uwepo wa madaktari hao ni fursa kubwa kwa wananchi wake hivyo amewasihi wananchi kujitokeza kwa wingi kupata huduma hiyo kwani hutokea mara chache kuwakuta wataalam kutoka hospitali mbalimbali wakiwa pamoja.

Bw. Assoumani ametoa shukrani za dhati kwa Rais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania Mhe Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuwezesha madaktari hao kutoa huduma, bila malipo yoyote.

Aidha Bw. Assoumani amesema kuwa serikali yake ipo tayari kutoa ushirikiano wa aina yoyote utakaotakiwa na madaktari hao ili mradi waweze kukamilisha kile ambacho kimewaleta hapa.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Saratani Ocean Road Dkt Diwani Msemo amemshukuru Bw. Assoumani kwa kuweza kufika katika kambi hiyo na kumuhakikishia kuwa hakuna mgonjwa hata mmoja wa Saratani atakaeachwa bila kupata huduma hata ikibidi kuchelewa kuondoka ili kukamilisha hayo.

Aidha Dkt. Msemo amemzawadia Bw. Assoumani Mgolole wa kimasai kama kielelezo cha ushujaa kwa kuchagua kusaidia wananchi wake kwa kukubali ujio wa kambi hii katika nchi yake huku akionesha ushirikiano wa hali ya juu kabisa.

Picha ya pili inaonesha Rais Assoumani katikati (mwenye suti ya bluu na miwani meusi) kushoto kwake ni Gavana wa kisiwa cha Anjoun akifuatiwa na Balozi wa Tanzania Comoro Mheshimiwa Saidi Yakubu pamoja na Dkt. Diwani Msemo, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Saratani Ocean Road, Kulia kwake ni Dr Peter Kisenge Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI pamoja na Dr Asha Mahita ambae ndie mratibu tiba utalii kutoka wizara ya Afya

Timu ya madaktari bingwa na ubingwa bobezi waingia nchini Comoro kutekeleza agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan

      Comments Off on

Timu ya madaktari bingwa na ubingwa bobezi waingia nchini Comoro kutekeleza agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan

Timu ya madaktari bingwa na ubingwa bobezi kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road inatarajia kuelekea Comoro kwaajili ya kutekeleza agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan la kupeleka madaktari hao katika Hospitali tofauti visiwani humo ili kuweza kuweka kambi maalum ya msaada wa huduma za kiuchunguzi na kimatibabu za Saratani.

Dkt. Diwani Msemo ambae ni mkurugenzi mtendaji wa Taasisi ya Saratani Ocean Road amesisitiza kuwa Taasisi ina wataalam wa kutosha ambao ni mabingwa bobezi kwenye upande wa Saratani hivyo wana uhakika wa huduma watakazokwenda kuzitoa huko hazina tofauti hata kidogo na zile zinazotolewa katika makao makuu ya Taasisi hiyo posta jijini Dar es Salaam.

Aidha Dkt. Msemo amewataka wananchi wa mji wa Anjouan kujitokeza kwa wingi katika kambi hiyo kwani huduma zitakazotolewa ni zenye ubora wa kimataifa na zitatolewa bila malipo yoyote.

Dkt. Msemo amezitaja Saratani zitakazofanyiwa uchunguzi kuwa ni zile za Matiti pamoja na Mlango wa kizazi kwa wakina mama, huku wakina baba wakifanyiwa uchunguzi na matibabu ya Saratani ya Tezi Dume.

Katika hatua nyingine, Dkt. Msemo amewatoa wasiwasi wakina baba kwa kuwajulisha kuwa uchunguzi wa Saratani kwa sasa hufanywa kwa njia rahisi mno ambapo inatolewa Damu kidogo kwenye kidole kama vinavyofanyika vipimo vya maleria kisha baada ya dakika Tano tu
Mtu anapata majibu yake, hivyo amesisitiza wakina baba kujitokeza kwa wingi katika Hospitali ya Howo ili kupata huduma hiyo.

Kambi hiyo maalum ya kimatibabu itafanyika kuanzia tarehe 05-12/10/2025, katika mji wa Anjouan unaopatikana Kisiwani Comoro.

Uongozi wa Taasisi ya Saratani Ocean Road umesema kuwa umejipanga kuwa kitovu cha Tiba utalii Africa</h4>

      Comments Off on

Uongozi wa Taasisi ya Saratani Ocean Road umesema kuwa umejipanga kuwa kitovu cha Tiba utalii Africa</h4>

Ambapo katika kurahisisha shughuli hiyo wamekutana na wadau wa sekta binafsi kutoka Global Medicare kujadili namna ya kushirikiana katika kuitikia wito wa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Akizungumza katika kikao hicho, Mkurugenzi Mkuu wa Global Medicare ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Taifa ya Tiba Utalii, Bw. Abdulmalick Mollel, amesema kuwa tiba utalii ni suala mtambuka linalohitaji ushirikiano mpana ili kufanikishwa.

Bw. Mollel amesisitiza kuwa Taasisi ya Saratani Ocean Road ina vigezo vyote vya kuwa kitovu cha tiba utalii kutokana na kuwa na wigo mpana wa wataalamu, miundombinu, na Teknolojia ya uchunguzi na matibabu ya saratani, si kwa Tanzania pekee bali pia kwa nchi jirani, hivyo ni muhimu kuboresha utoaji huduma, kuleta ubunifu katika huduma, na kutangaza huduma hizo ndani na nje ya nchi.

Bw. Mollel pia amempongeza Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo, Dkt. Diwani Msemo, kwa kasi yake ya utekelezaji na maboresho makubwa ya miundombinu na huduma, ambayo yamepewa kipaumbele katika Mpango Mkakati wa 2025–2030, ambapo Taasisi inalenga kupata ithibati za kimataifa kwa huduma zake za Vipimo na matibabu.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Saratani Ocean Road, Dkt. Diwani Msemo, amemshukuru Bw. Mollel kwa utayari wake wa kushirikiana na Taasisi katika kuandaa mpango mkakati wa tiba utalii ambao utaongeza idadi ya wagonjwa kutoka nje. Katika mwaka 2024, kwani zaidi ya wagonjwa 384 kutoka Zambia, Malawi, Comoro, Kenya, Msumbiji na Burundi walipata huduma katika Taasisi hiyo.

Dkt. Msemo amesema Mpango mkakati unaoandaliwa unalenga kuitikia wito wa Rais Samia Suluhu Hassan wa kuimarisha tiba utalii nchini.

Dkt. Msemo amesisitiza kuwa menejimenti na wafanyakazi wa Taasisi wanapaswa kuwa tayari kubadili mitazamo yao, kujifunza, na kushirikiana na wenzao wenye uzoefu kutoka sekta binafsi na serikali katika tiba utalii.

Ajenda ya kukuza tiba utalii nchini Tanzania imeanzishwa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, na ni miongoni mwa Vipaumbele vya Taasisi hii.

Maadhimisho ya siku ya wauguzi ngazi ya tawi la Ocean Road

      Comments Off on

Maadhimisho ya siku ya wauguzi ngazi ya tawi la Ocean Road

“Wauguzi wanatakiwa kuiga falsafa za Florence Nightingale” hayo ameyasema leo Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Saratani Ocean Road Dkt. Diwani Msemo katika maadhimisho ya siku ya wauguzi ngazi ya tawi la Ocean Road yaliyofanyika katika viwanja vya Taasisi hiyo.

Dkt. Msemo amewataka wauguzi kufanya kazi kama Florence Nightingale alivyokuwa akifanya ikiwemo kuwa na moyo wa huruma kwa wagonjwa.

Pamoja na hayo Dkt. Msemo ametoa nyongeza ya zawadi ya Mkurugenzi ya shilingi laki moja kwa Kila mfanyakazi bora waliopata zawadi katika maadhimisho hayo.

Vile vile ametoa ahadi ya kutatua changamoto zinazowakumba wauguzi kadiri Taasisi inavyokuwa na uwezo wa kutatua changamoto hizo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa uuguzi wa Taasisi ya Saratani Ocean Road Bi. Mary Haule amesema muuguzi anatakiwa kutoa huduma za uuguzi kwa uadilifu wa hali ya juu.

Bi. Haule amekumbusha kuwa uuguzi ni moyo wa Taasisi na ndio sura ya Taasisi na wauguzi wanatakiwa kuhakikisha wanalinda sura ya Taasisi.

Vile vile Mwenyekiti wa TANNA tawi la Taasisi ya Saratani Ocean Road Bi. Herrieth Mbwana amesema tarehe 12 Mei Kila mwaka ndio maadhimisho ya siku ya wauguzi Duniani, na tarehe 23 mei ndio kilele Cha maadhimisho ya kudumisha muasisi na muanzilishi wa uuguzi Duniani Bi. Florence Nightingale.

WANANCHI ZAIDI YA 900 PERAMIHO WAPATIWA HUDUMA ZA SARATANI BILA MALIPO

      Comments Off on

WANANCHI ZAIDI YA 900 PERAMIHO WAPATIWA HUDUMA ZA SARATANI BILA MALIPO

Na WAF – Songea, Ruvuma

Wananchi zaidi ya 900 wamepatiwa huduma za uchunguzi na matibabu ya ugonjwa wa saratani bila malipo katika Hospitali ya MT. Joseph Peramiho, huduma ambazo kutolewa na madaktari bingwa wa magonjwa ya saratani kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road kwa muda wa siku nne (4).

Waziri wa Afya Mhe. Jenista Mhagama amesema hayo leo Aprili 19, 2025 alipotembelea kambi maalum ya uchunguzi wa magonjwa ya saratani ikiwemo saratani ya matiti na tezi dume katika Hospitali ya Mtakatifu Joseph Peramiho Mkoani Ruvuma inayoendelea hadi tarehe 20 Aprili, 2025 ikiwa leo ni siku ya tano (5).

“Watu 18 wamegundulika kuwa na viashiria vya ugonjwa huo ambapo 12 ni wanawake ambao tayari wameshapatiwa matibabu na sita (6) ni wanaume ambao wamepewa rufaa ya kwenda kufanyiwa uchunguzi zaidi, tuna kila sababu ya kumshukuru sana Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kufanya haya yote kwa sababu ya kujali uhai wa maisha ya Watanzania,” amesema Waziri Mhagama.

Aidha, Waziri Mhagama amesema taarifa ya utafiti ya Tume ya Saratani (Oncology Commission Report) iliyozinduliwa nchini tarehe 26 Septemba, 2022 ilionesha kwamba nchi zilizopo kusini mwa jangwa la Sahara ziko hatarini kupata idadi kubwa ya vifo kutoka 520,348 hadi 1,000,000 kufikia mwaka 2030 endapo hatua madhubuti hazitachukuliwa.

“Takwimu za Taifa kwa miaka mitano (5) kuanzia mwaka 2019 – 2024 zinaonesha kuwa aina za saratani zinazoongoza ni saratani ya mlango ya kizazi kwa asilimia 41, saratani ya matiti kwa asilimia19, saratani ya utumbo mkubwa na mdogo kwa asilimia 6.1, saratani ya koo kwa asilimia5.7 pamoja na saratani ya kichwa na shingo kwa asilimia 4.3,” amesema Waziri Mhagama.

Katika kuendelea kujikinga na magonjwa hayo, Waziri Mhagama amewataka wananchi kuchukua hatua kwa kuzingatia ulaji unaofaa ikiwemo kupunguza ulaji wa vyakula vyenye mafuta mengi, chumvi nyingi na sukari, kuacha tabia bwete, kuacha vilevi pamoja na kuwa na tabia za kupima afya zao.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Saratani Ocean Road Dkt. Diwani Msemo amesema lengo la kambi hiyo maalum ni kutoa elimu inayosababisha saratani, uchunguzi wa saratani za awali pamoja na matibabu yake kwa wananchi.

“Kutokana na ushirikiano tulioupata katika hospitali hii, tumeamua kuwachukua wataalam kama wanne (4) hapa twende nao Ocean Road tukawafundishe namna ya kutoa huduma za saratani ili waje waendelee kutoa huduma hizo hapa kwakuwa pia kuna wagonjwa wanaokuja hapa kutoka nchi jirani.

Naye, shuhuda wa ugonjwa wa Saratani Bw. Cedou Mandingo (Babuu wa kitaa) amewashauri wananchi kuchukua hatua za haraka kwa kuchunguza afya zao mara kwa mara iwapo ikigundulika wana viashiria vya ugonjwa huo ili kuwahi mapema kupata matibabu kwakuwa ugonjwa huo unatibika na unapona.

“Ni jukumu letu sisi mabalozi tuwe na utaratibu wa kwenda katika vituo vya afya kutoa elimu ili wananchi wengi wajitokeze kufanya uchunguzi wa Saratani, mimi sijapona saratani kwa waganga wa nje ya nchi, nimepona hapa hapa nchini sababu ya uwepo wa watalam wa afya wabobezi waliowezeshwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hasaan, amini kwamba saratani inatibika na unapona ukiwahi mapema,” amesema Bw. Mandingo.

Shuhuda wa ugonjwa wa Saratani Bw. Cedou Mandingo (Babuu wa kitaa) ambae ni mtangazaji wa Cloud Media ameiomba Serikali kuipa jina jengo la Nuclear Medicine Pet-Ct Scan kuitwa Samia Suluhu Pet-Ct Scan ili kuonesha heshima na kumshukuru Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa uwekezaji wa mashine kubwa ya kupima saratani katika Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI).

Babuu wa kitaa ametoa ombi hilo leo Aprili 19, 2025 wakati akitoa ushuhuda wa kupona ugonjwa wa saratani ambapo amepata matibabu ndani ya nchi chini ya madaktari bigwa kutoka katika Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI) na kuwataka wananchi wajitokeze mapema kufanya uchunguzi wa afya zao.

“Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amefanya mageuzi makubwa ndani ya nchi hii katika upande wa Sekta ya Afya na hasa kwenye upande wa magonjwa ya saratani kwa muda mchache, Mhe. Waziri Jenista Mhagama nakuunga mkono kwa kumuongezea vyeo Rais kwa kumuita Daktari bigwa, mbobezi na nambari moja,” amesema Babuu wa kitaa

Waziri wa afya Mhe. Jenista Mhagama ametembelea katika Taasisi ya Saratani Ocean Road kuona utoaji huduma za tiba mionzi

      Comments Off on

Waziri wa afya Mhe. Jenista Mhagama ametembelea katika Taasisi ya Saratani Ocean Road kuona utoaji huduma za tiba mionzi

Waziri wa afya Mhe. Jenista Mhagama ametembelea katika Taasisi ya Saratani Ocean Road kuona utoaji huduma za tiba mionzi zinavyoendelea katika Taasisi kwa wagonjwa wa saratani.

Mh. Mhagama amejionea kukamilika kwa matengenezo ya mashine ya LINAC ambayo ilipata changamoto leo asubuhi na kupongeza uongozi wa Taasisi kwa kuhakikisha mashine inafanya kazi ili kuondoa usumbufu kwa wagonjwa.

Mhe Waziri amepongeza kwa kutengenezwa kwa mashine hiyo moja iliyokuwa inasumbua

Hata hivyo, Mhe. Mhagama ameongea na wagonjwa mbalimbali wanaopata huduma katika Taasisi na kuingeza kuwa, serikali ipo mbioni kuongeza mashine nyingine ya Tiba mionzi ili kuondoa shida zinazotokana na uchache wa mashine.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Saratani Ocean Road Dkt. Julius Mwaiselage ameishukuru serikali kwa kufanya mchakato wa kuongeza mashine nyingine ya Tiba mionzi itakayokuja hivi karibuni kwani wagonjwa wa saratani wamekuwa wengi kuhitaji huduma za tiba mionzi.

Naibu waziri mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Doto Biteko amezindua mpango kazi wa Taifa wa haki na ustawi wa watu wenye Ualbino (MTHUWWU)

      Comments Off on

Naibu waziri mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Doto Biteko amezindua mpango kazi wa Taifa wa haki na ustawi wa watu wenye Ualbino (MTHUWWU)

Naibu waziri mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Doto Biteko amezindua mpango kazi wa Taifa wa haki na ustawi wa watu wenye Ualbino (MTHUWWU) na mkakati wa Taifa wa Teknolojia saidizi.

Akizungumza katika maadhimisho ya kilele cha siku ya watu wenye ulemavu nchini, yaliyofanyika katika ukumbi wa Diamond jubilee uliopo Upanga jijini Dar es salaam, Dkt.Biteko amesema kuwa, mpango huu uliozinduliwa naye, ni muhimu kufuatiliwa na kuhakikisha umefanikiwa kwani watu wote nchini ni walemavu watarajiwa na hatujui lini tutapatwa na madhila hayo.

Dkt. Biteko amewaagiza wakuu wa mikoa yote nchini kuhakikisha kuwa wanasimamia maagizo hayo katika maeneo yao ya kazi kwani kwa upande wao ni rahisi mno kwakuwa wapo karibu sana na jamii.

Taasisi ya Saratani Ocean Road nayo imeshiriki katika shughuli hiyo kama mdau mkubwa wa watu wenye Ualbino ambapo imetoa mafuta kwa watu wenye ualbino waliobahatika kutembelea katika banda letu huku wakitoa elimu mbalimbali pamoja na vipeperushi ili kuwapa watu nafasi ya kujifunza mambo mengi kuhusu ualbino

Dkt. Maguha Stephano ambae ni meneja wa huduma za kinga katika Taasisi ya Saratani Ocean Road amesema kuwa mafuta hayo yametolewa bila malipo yoyote huku akiendelea kuwaasa wananchi kusogea katika banda hilo ili kujipatia mafuta hayo pamoja na kujifunza mambo mengine mengi yanayohusiana na saratani pamoja na ualbino.