Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mheshimiwa Dkt. Dorothy Gwajima akiwa ziara ya kikazi katika Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI), amepongeza jitihada kubwa za uboreshwaji wa huduma na upatikanaji wa dawa za kutibu saratani uliokua kutoka asilimia 4 mwaka wa fedha 2014/2015 na kufikia asilimia 96 kwa mwaka wa fedha 2019/2020.
Mheshimiwa Waziri Mheshimiwa Dkt. Dorothy Gwajima akiwa katika ziara ya kikazi ORCI, amesema kuwa lengo lake ni kujionea hali ya utoaji wa huduma, changamoto na mwelekeo kwa ujumla pamoja na kuwapongeza na kuwatakia utekelezaji mwema wa ilani ya chama tawala katika awamu ya tano wataalamu wote wa afya nchini hususani mabingwa katika ngazi zote.
Mheshimiwa Waziri Dkt. Dorothy amesifu hatua zinazochukuliwa na Taasisi ya saratani katika kupunguza idadi ya rufaa za nje ya nchi kutokana na huduma hizo kupatikana hapa nchini, pamoja na kuongezeka kwa idadi ya wagonjwa wa mataifa ya nchi jirani wanaofika na kutibiwa katika Taasisi ya Saratani Ocean Road, amesema, azma ya Serikali ni kuzifanya Taasisi zetu ziwe na uwezo wa kipekee wa kutoa huduma bora zinazoweza kuwavuta raia wa mataifa makubwa kuja kutibiwa katika mahospitali yetu nchini. Pia, amesifu kwa Kiasi kikubwa utekelezaji wa ilani ya chama tawala kwa kusaidia idadi kubwa ya wananchi wasio na uwezo wa kulipia matibabu ya saratani kwa kutoa misamaha ya dawa na matibabu. Misamaha kwa wanufaika iliyotolewa na Taasisi iliongezeka kutoka wanufaika 194,470 mwaka 2015/16 hadi kufikia wanufaika 495,538 mwaka 2019/20
Mkurugenzi wa Taasisi ya Saratani Ocean Road Dkt. Julius Mwaiselage awali ya yote, alimkaribisha Waziri Gwajima, na kumpongeza kwa kuteuliwa kwake kuwa mbunge na kisha kuwa Waziri wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, ambapo alimuahidi kuwa ORCI itashirikiana naye kuhakikisha kuwa malengo ya Serikali na ilani ya Chama Tawala yanatekelezwa kwa ufanisi.
Mkurugenzi Dkt. Mwaiselage alielezea mafanikio na changamoto mbalimbali zinazoikabili Taasisi ya Saratani pamoja na mikakati inayofanywa kukabili changamoto hizo. Ambapo, alimuomba Mheshimiwa Waziri kusaidia katika utatuzi wa changamoto ambazo upo katika ngazi ya Wizara ikiwamo utozwaji wa kodi wa vipuri vya vifaa tiba vinapoingizwa nchini kwa ajili ya kutengeneza vifaa tiba na pia ucheleweshwaji wa utoaji wa dawa na vifaa tiba hivyo
Mheshimiwa Waziri Dkt. Dorothy Gwajima akiwa na Mkurugenzi wa Taasisi ya Saratani Ocean Road wakitembelea kuangalia utendaji kazi wa duka la dawa OCP.